This is default featured slide 1 title

Go to Blogger edit html and find these sentences.Now replace these sentences with your own descriptions.

This is default featured slide 2 title

Go to Blogger edit html and find these sentences.Now replace these sentences with your own descriptions.

This is default featured slide 3 title

Go to Blogger edit html and find these sentences.Now replace these sentences with your own descriptions.

This is default featured slide 4 title

Go to Blogger edit html and find these sentences.Now replace these sentences with your own descriptions.

This is default featured slide 5 title

Go to Blogger edit html and find these sentences.Now replace these sentences with your own descriptions.

Monday, July 10, 2017

AITEL NA GSMA WANDAA MASHINDANO YA SULUHU ZA MFUMO A MALIPO YA PESA KUPITIA SIMU ZA MKONONI

DAR ES SALAAM.
Kampuni ya simu za mkoni ya Airtel Tanzania kwa kushirikiana na GSMA wameandaa mashindano ya suluhu za mfumo wa malipo ya pesa kupitia simu za mkononi ambayo yanafanyika jijini Dar es Salaam kwa mwaka wa pili mfululizo.
Mashindano hayo ambayo yamedhaminiwa na Airtel money na Comviva wakishirikiana na muungano wa mashirika ya simu za mkononi ulimwenguni GSMA yanajumuisha washiriki kutoka Africa. Wajasiriamali wa TEKNOHAMA kutoka Ghana, Kenya, Uganda na Tanzania watachuana kutengeza suluhu kwenye maeneo makuu matatu, yaani malipo kwenye sekta ya usafirishaji, mfumo wa malipo ya jumla (bulk payment )na mfumo wa malipo ya pochi ya Comviva na Airtel yaani ( Airtel Comviva mobile wallet).  
Tanzania imepata fursa ya kuandaa mashindano hayo kwasababu inajulikana kama kiongozi katika sekta ya simu za mkononi inayoongoza katika kujenga mifumo ya malipo ya simu ( mobile money payment) Hivyo ni fursa ya kipekee kwa wajisiriamali wa kitanzania kuweza kutengeneza suluhu za mifumo ya malipo ya simu za mkononi zitakazotumika barani Africa.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo, Mkurugenzi wa Masoko Airtel Tanzania Isack Nchunda alisema ushirikiano huu ni muhimu kwa vile unawezesha wajasiriamali wa TEKNOHAMA kuja na suluhu ambayo itaweza kusaidia kufanya malipo kupitia simu za mkononi kwa haraka na hivyo kuokoa kupoteza muda kupanga foleni kusubiria kufanya malipo.
Sisi Airtel Tanzania tumekuwa msitari wa mbele kuwezesha wajasiriamali kwa njia mbali mbali. Kwa kupitia mashindano tunaendeleza uwezeshaji huo kwani kwa kila suluhu itakayopatikana haitaishia hapa mbali itaendelea kuboresha na kuwekwa kwenye mfumo wa malipo ya simu za mkononi, alisema Nchunda.
Kwa upande wake, Mkuu wa kitengo cha Teknohama GSMA Gareth Pateman alisema washiriki wa mashindano hayo wanaweza kutengeneza suluhi moja au mbili katika zile tatu huku mshindi akipata ticketi ya kwenda Barcelona, Spain huku akiwa amelipiwa gharama zote.
Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Airtel Tanzania, Isack  Nchunda, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana baada ya ufunguzi wa mashindano ya suluhu za mfumo wa malipo ya pesa kupitia simu za mkononi yanayodhaminiwa na Airtel money na Comviva wakishirikiana na muungano wa mashirika ya simu za mkononi ulimwenguni GSMA.

Sunday, July 2, 2017

MAMLAKA YA UDHIBITI WA UNUNUZI KATIKA SEKTA YA UMMA (PPRA) KATIKA MAONESHO YA SABASABA 2017

Meneja Usimamizi na Utawala waMifumo ya TEHAMA, wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi katika Sekta ya Umma (PPRA), Bw.Bernard Ntelya, (kulia), akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensehni wa PPF, Bw. William Erio, alipotembeela banda la Mamlaka hiyo Julai 2, 2017.

NA K-VIS BLOG/Khalfan Said
MAMLAKA ya Udhibiti wa Ununuzi katika Sekta ya Umma, (PPRA), kama zilivyo taasisi nyingine za serikali, imeweka banda lake kwenye jingo la Wizara ya Fedha na Mipango, wakatihuuwa maonesho ya 41 ya biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere, barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.

Viongozi na maafisa wa juu wa serikali wamepata fursa ya kutembelea banda hilo ili kujua huduma wanazotoa kwenye banda hilo, ambapo maafisa wa PPRA, wamekuwa wakitoa elimu na kugawa vipeperushi vyenye maeelzo mbalimbali ya kazi za Mamlaka hiyo, lakini na taarifa zinazoeleza sheria ya manunuzi ya umma na umuhimu wake.

Mamlaka hiyo imeanzishwa kwa sheria ya manunuzi ya Umma CAP 410 kama ilivyobadilishwa na Sheria ya Manunuzi ya Umma ya namba 7 ya mwaka 2011 ambayo inatoa Mamlaka ya kusimamia manunuzi ya umma kwa taasisi zote za Umma (Serikali), upande wa Tanzania Bara.

Kwa mujibu wa maafisa wa PPRA walioko kwenye banda hilo, wanasema, malengo makuu ya PPRA ni kuhakikisha manunuzi yote kwenye taasisi za umma, yanafanyika kwa usawa katika shindani, uwazi, bila unyanyasaji ili mwisho wa siku watoa huduma watoe huduma inayolingana na thamani ya fedha wanazolipwa kwa maendeleo ya taifa, (Value for Money).

Aidha wamesema, PPRA inao wajib u wa kuweka viwango katika mfumo wa manunuzi ya umma katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (upande wa Tanzanai Bara).


Afisa Mwandamizi wa PPRA, Bw. Mcharo Mrutu, (kulia), akimpatia vipeperushi vyenye taarifa mbalimbali za PPRA, Mkurugenzi Mkuu wa PPF, Bw. William Erio
Bw. Mrutu, (kulia), akizungumza na Mwananchi huyu aliyetembelea banda la Mamlaka hiyo
Bw. Ntelya(kulia), akifafanua jambo kwa mwananchi huyu aliyefika kujua shughuli za PPRA

Monday, March 20, 2017

AIRTEL KUZINDUA MADUKA ZAIDI YA 2000 TANZANIA

·        Wateja wa Airtel kupata huduma kwa haraka na karibu zaidi
·        Mradi huu utachochea upatikanaji wa huduma za kifedha
·        Airtel yaendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuendelea kuwekeza nchini
Shinyanga 
Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania leo imetangaza mpango wake wa kuzindua ma duka Saidi ya 2000 nchini utakaowawezesha wateja wake  kupata huduma na bidhaa zake za kibunifu kwa urahisi zaidi

maduka haya ya Airtel yatakuwa na muonekano unaofanana na yatakuwa katika maeneo maalumu ambayo yatawawezesha maelfu ya wakazi kupata huduma kirahisi na kukidhi mahitaji yao kwa ufanisi zaidi

Maduka hayo yatatoa huduma mbalimbali zikiwemo huduma za kifedha, huduma za intaneti, kuongeza salio , kusajili namba na pia kuunganisha wateja wapya kwenye mtandao wa Airtel

Katika kutekeleza mpango huo wa Airtel imezindua maduka 8 katika mkoa wa Shinyanga kwenye uzinduzi uliofanywa na Mkuu wa wilaya ya Shinyanga kwa kushirikiana na Mkurugenzi Mkuu wa Airtel ambapo Airtel imeeleza mpango wake wa kujitanua zaidi na ili kufikisha huduma zake karibu na watanzania waishio mjini na pembezoni ya nchi

Akiongea wakati wa uzinduzi maduka hayo mkoani Shinyanga, Mkurugenzi Mkuu wa Airtel, Bwn Sunil Colaso alisema” tunajisikia fahari kutangaza azma yetu kubwa itakayowezesha upatikanaji wa bidhaa na huduma zetu kirahisi zaidi na kuendelea kuthibitisha dhamira yetu ya kuwapatia wateja wetu huduma bora. leo tunazindua maduka 8 hapa shinyanga na mpango wetu ni kuwa na jumla ya maduka yapatayo 76 mkoani hapa

Tunaamini hii ni njia pekee ya kuwafikia wateja wetu kujua changamoto zao na kuzitatua kwa wakati na vilevile kuwaunganisha na huduma na bidhaa zetu za kipekee na kibunifu zinazosaidia kutatua changamoto zao za kila siku za kijamii na kiuchumi. Mpango wetu ni kuwa na maduka kama haya takribani 2000 nchi nzima na tayari tumeshaanza kufungua maduka haya kwa kasi katika maeneo mbalimbali nchini. Aliongeza Colaso

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Bi Josephine Matiro alisema” Tunafurahi kuona juhudi zinazofanywa na Airtel katika kusogeza huduma zake na wateja wake lakini  pia kutengeneza ajira kwa wengi. Tunaamini maduka yanayozinduliwa leo hapa Shinyanga na yale yatakayozinduliwa mbeleni yatachochea kwa kasi kwa huduma za kifedha kupitia simu za mkononi kwa urahisi na kwa usalama na kutoa mwanya kwa Maendeleo Mengi kuku a kiuchumi. Napenda kuwahamasisha wamiliki wa maduka kutumia fursa hii kutanua biashara zenu na kutengeneza ajira kwa vijana hapa mkoani Shinyanga.


Kuanzishwa kwa maduka haya sehemu mbalimbali nchini kunathibitisha kwa vitengo dhamira ya Airtel kuendelea kuwekeza nchini na Afrika kwa ujumla
 Meneja  Mauzo wa Airtel Shinyanga, James Moilo (kushoto) akimuonyesha Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga , Josephine Matiro  moja kati ya simu za Smartphone zinazopatikana katika moja kati ya maduka wakati Airtel ilipozindua duka la huduma kwa wateja mkoani Shinyanga. Akishuhudia ni Mkurugenzi Mkuu wa Airtel Tanzania, Bwn Sunil Collaso

 Mkurugenzi Mkuu wa Airtel Tanzania, Bwn Sunil Collaso akibadilishana mawazo na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga , Josephine Matiro  kabla ya uzinduzi wa duka mkoani hapo
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga , Josephine Matiro  akiwapongeza wa Airtel kwa kuuanzisha mpango wa kufungua maduka zaidi ya 76 na kufikisha huduma kwa wateja kwa urahisi mkoani shinyanga

Tuesday, January 31, 2017

KAULI YA SERIKALI BUNGENI KUHUSU MWENENDO WA HALI YA UCHUMI WA TAIFA

KAULI YA SERIKALI BUNGENI KUHUSU MWENENDO

WA HALI YA UCHUMI  WA TAIFA



UTANGULIZI



  1. Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya Bunge Na. 49 (1 ) ya Kanuni za Bunge toleo la Januari mwaka 2016, naomba kuwasiisha taarifa kuhusu hali ya uchumi  wa Taifa, hususan mwenendo wa viashiria mbalimbali vya uchumi, ikiwemo ukuaji wa uchumi, mfumuko wa bei, mwenendo wa sekta ya nje na akiba ya fedha za kigeni, mwenendo wa sekta ya fedha ikiwa pamoja na hali ya ukwasi na deni la Taifa.

  2. Mheshimiwa Spika, Serikali inatoa taarifa hii ili kukitaarifu chombo hiki muhimu cha wawakilishi wa wananchi kuhusu afya ya uchumi wa Taifa letu ili Waheshimiwa Wabunge waweze kuwafikishia wananchi ujumbe/maelezo sahihi badala ya uvumi wa mitaani.
             
    Ukuaji wa Pato la Taifa

  3. Mheshimiwa Spika, ukuaji wa uchumi ni mojawapo ya viashiria vinavyotazamwa katika kutathmini afya ya uchumi wa Taifa. Ukuaji wa uchumi unapimwa kwa kutumia ukuaji wa Pato la Taifa yaani thamani ya bidhaa na huduma zilizozalishwa katika nchi katika kipindi kinachorejewa ikilinganishwa na kipindi kilichopita. Takwimu za ukuaji wa Pato la Taifa zinaonesha kuwa uchumi wa Taifa umeendelea kukua na Tanzania imebaki kuwa miongoni mwa nchi za bara la Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ambazo uchumi wake unakua kwa kasi kubwa zaidi. Naomba niwape mifano ya nchi jirani kama ifuatavyo.

    Jedwali1: Ukuaji wa Pato la Taifa Katika Baadhi ya Nchi za Kiafrika


NCHI

2015

2016 (Matarajio)

Burundi

-4.0

-0.5

Kenya

5.6

6.0

Rwanda

6.9

6.0

Tanzania

7.0

7.2

Uganda

4.8

4.9

Zambia

3.0

3.0

Malawi

2.9

2.7

Congo DRC

6.9

3.9

Afrika Kusini mwa Sahara

3.4

1.4



  1. Mheshimiwa Spikakatika kipindi cha Januari hadi Septemba, 2016 kiwango halisi cha ukuaji wa Pato la Taifa kiliongezeka na kufikia wastani wa asilimia 6.5 ikilinganishwa na kiwango cha ukuaji cha asilimia 6.3 katika kipindi kama hicho mwaka 2015. Kwa ujumla, sekta nyingi zilikua kwa kasi isipokuwa sekta chache. Sekta zifuatazo zilikuwa na viwango vikubwa vya ukuaji katika kipindi hicho: shughuli za uchimbaji madini na mawe (asilimia 15.8); shughuli za usafirishaji na uhifadhi wa mizigo (asilimia 15.5); habari na mawasiliano (asilimia 13.4); na huduma za fedha (asilimia 11.5).

  2. Mheshimiwa Spika, maoteo ya ukuaji wa Pato la Taifa kwa mwaka 2016 (Januari-Desemba) yalitarajiwa kuwa asilimia 7.2. Hata hivyo, uchambuzi uliofanywa na Serikali kushirikiana na Shirika la Fedha za Kimataifa (IMF) unaonesha kuwa ukuaji wa uchumi tulioutegemea unaweza usifikiwe. Matarajio ya sasa ni kufikia ukuaji wa wastani wa asilimia 7.0. Hii inatokana na mwenendo wa uchumi katika miezi tisa ya mwanzo ambapo sekta zinazoajiri watu wengi na zenye mchango mkubwa katika uchumi hazikukua katika kasi iliyotarajiwa ikiwemo sekta ya kilimo ambayo ilikua kwa wastani wa asilimia 2.1 (matarajio ya mwaka ni asilimia 2.6) na biashara ilikua kwa wastani wa asilimia 5.6 (matarajio ya mwaka ni asilimia 7.6).  Aidha, kuzorota  kwa uchumi kwa nchi za Jumuiya ya Ulaya na China ambao ni wabia wetu wakubwa wa biashara na uwekezaji ndio kumechangia kupunguza matarajio ya awali ya kasi ya ukuaji  wa uchumi nchini. Kasi ya ukuaji wa uchumi wa China inakadiriwa kupungua kutoka asilimia 6.9 mwaka 2015 hadi asilimia 6.6 mwaka 2016.

    Mfumuko wa bei

  3. Mheshimiwa Spika, kiashiria kingine cha jumla cha afya ya uchumi wa Taifa ni mfumuko wa bei ambao unapima mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zinazotumiwa na kaya nchini. Mfumuko wa bei ulipungua kutoka asilimia 6.5 Januari 2016 hadi asilimia 5.5 Juni 2016 na kupungua zaidi hadi asilimia 4.5 Septemba 2016 na baadaye kupanda kidogo mwezi Desemba na kufikia asilimia 5.0. Aidha, mfumuko wa bei kwa mwaka mzima wa 2016 ulipungua na kufikia wastani wa asilimia 5.2 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 5.6 mwaka 2015. Maana yake ni kuwa bei za bidhaa na huduma ziliongezeka kwa kasi ndogo zaidi ikilinganishwa na kipindi cha nyuma. Mwenendo huu wa kushuka mfumuko wa bei ulichangiwa na kasi ndogo ya ongezeko la bei za chakula nchini, kushuka kwa wastani wa bei za mafuta ya petroli katika soko la dunia, utekelezaji madhubuti wa sera za bajeti na fedha, na utulivu wa thamani ya Shilingi ya Tanzania dhidi ya dola ya kimarekani.

  4. Mheshimiwa Spika,  mfumuko wa bei unatarajiwa kuendelea kubakia katika viwango vya tarakimu moja katika siku zijazo na kubakia ndani ya lengo la muda wa kati la asilimia 5.0. Matarajio haya yatategemea kuendelea kutulia kwa bei ya nishati nchini kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya gesi asilia katika uzalishaji wa umeme, mwendelezo wa sera thabiti ya fedha na kibajeti, kutobadilika sana kwa bei za mafuta katika soko la dunia, pamoja na kuendelea kuwepo kwa utulivu wa thamani ya Shilingi. Hata hivyo, kuna viashiria vinavyoonesha uwezekano wa kuongezeka kwa mfumuko wa bei kutokana na hali ya ukame uliojitokeza hapa Tanzania na kwa baadhi ya nchi za ukanda wa nchi za  Afrika Mashariki pamoja na uwezekano wa kuongezeka kwa bei za mafuta katika soko la dunia.



Mfumuko wa bei katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki



  1. Mheshimiwa Spika, wastani wa mfumuko wa bei kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki uliendelea kuwa imara na kubakia katika wigo wa tarakimu moja mwaka 2016. Nchini Kenya, mfumuko wa bei ulipungua kufikia wastani wa asilimia 6.3 mwaka 2016 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 6.6 mwaka 2015. Hata hivyo, mfumuko wa bei nchini Uganda ulipanda na kuwa asilimia 5.4 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 5.2 mwaka 2015.

    Thamani ya shilingi

  2. Mheshimiwa Spika, kiashiria kingine cha afya ya uchumi ni uimara wa thamani ya shilingi. Katika kipindi cha Julai – Desemba 2016, Serikali iliendelea na utekelezaji wa sera za fedha na bajeti, hatua zilizowezesha kuimarika kwa thamani ya shilingi dhidi ya Dola ya Kimarekani. Katika kipindi hicho,  thamani ya shilingi dhidi ya Dola ya Kimarekani ilipungua kwa kasi ndogo kutoka wastani wa shilingi 2,144.27 kwa dola moja mwezi Desemba 2015 hadi shilingi 2,170.44 kwa dola moja mwezi Desemba 2016. Kuimarika kwa thamani ya shilingi kulitokana na hatua mbalimbali za sera ya fedha zilizochukuliwa na Benki Kuu katika kusimamia hali ya ukwasi kwenye uchumi pamoja na kuimarika kwa urari wa bidhaa na huduma katika sekta ya nje.  Aidha, thamani ya Shilingi kwa Dola ya Kimarekani ilishuka (kwa takriban asilimia 2.15 katika kipindi cha miezi kumi na mbili kufikia tarehe 19 Januari 2017), kufuatia kuimarika kwa Dola ya Kimarekani. Kuimarika kwa Dola ya Kimarekani kuliathiri pia sarafu nyingine zikiwemo yuan ya China (iliyoshuka thamani kwa asilimia 3.55 katika kipindi cha miezi kumi na mbili kufikia tarehe 19 Januari 2017), shilingi ya Uganda (asilimia 3.7), Faranga ya Rwanda (asilimia 8.55), na Pauni ya Uingereza (iliyoshuka thamani kwa asilimia 13.04).

  3. Mheshimiwa Spika, kuimarika kwa Dola ya Kimarekani kulitokana zaidi na kupanda kwa riba ya sera ya fedha (policy rate/Fed Fund rate) mwezi Desemba 2016, hali iliyosababisha wawekezaji kuongeza mahitaji yao ya Dola ya Kimarekani kwa ajili ya kuwekeza. Aidha, kwa upande wa Tanzania mwezi Januari ni msimu wa mapato madogo ya fedha za kigeni zitokanazo na mauzo ya mazao ya biashara, hali ambayo imechangia pia kuwa na dola pungufu kwenye soko la fedha.





Sekta ya Nje na Akiba ya Fedha za Kigeni



  1. Mheshimiwa Spika, hali ya uchumi inatathminiwa pia kwa kuangalia mwenendo wa biashara ya nje na akiba ya fedha za kigeni. Katika mwaka 2016, nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa, huduma na uhamishaji mali nchi za nje (current account deficit) ilipungua kwa asilimia 48.8 na kufikia nakisi ya Dola za Kimarekani milioni 2,054.8, kutoka nakisi ya Dola za Kimarekani milioni 4,011.6 kwa mwaka 2015. Kupungua huko kulitokana zaidi na ongezeko la thamani ya madini hususan dhahabu, bidhaa asilia, mapato yatokanayo na utalii, pamoja na kupungua kwa thamani ya bidhaa zilizoagizwa kutoka nje ya nchi hususan bidhaa za kukuza mitaji, na bidhaa za matumizi ya kawaida. Katika kipindi hicho, thamani ya bidhaa na huduma zilizouzwa nje ya nchi ziliongezeka kwa asilimia 5.2 na kufikia Dola za Kimarekani milioni 9,381.6 wakati thamani ya bidhaa na huduma toka nje zilipungua kwa asilimia 13.7 na kufikia Dola za Kimarekani milioni 10,797.4

  2. Mheshimiwa Spika, hadi mwezi Desemba 2016, akiba ya fedha za kigeni ilifikia Dola ya Kimarekani milioni 4,325.6 ambazo zinatosheleza kuagiza bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa takriban miezi 4.2. Aidha, rasilimali za fedha za kigeni za mabenki ya biashara zilifikia Dola ya Kimarekani milioni 768.2, wakati amana za fedha za kigeni zilizohifadhiwa na wakazi katika benki za biashara zilifikia Dola za Kimarekani milioni 2,870.8. Hivyo, akiba ya fedha za kigeni imeendelea kuwa ya kuridhisha.

    Mwenendo wa Sekta ya Kibenki

  3. Mheshimiwa Spika, kiashiria kingine cha hali ya uchumi ni mwenendo wa sekta ya fedha. Katika kipindi kilichoishia Desemba 2016, tathmini ya hali ya mabenki yetu na taasisi za fedha inaonesha kuwa mabenki yetu ni imara na salama, yakiwa na mitaji na ukwasi wa kutosha: Kiwango cha mitaji kikilinganishwa na mali iliyowekezwa (total capital to total risk weighted assets and off-balance sheet exposures) kilikuwa asilimia 17.8 kikilinganishwa na kiwango cha chini kinachotakiwa kisheria cha asilimia 10.0.

    Hali ya Ukwasi katika uchumi

  4. Mheshimiwa Spika, ukwasi (liqudity) ni kiasi cha fedha kilichopo katika uchumi na unajumuisha fedha taslim, amana katika mabenki zilizopo Benki Kuu. Utoshelevu wa ukwasi katika uchumi unapimwa kwa kuangalia viashiria mbalimbali ikiwemo ujazi wa fedha, mwenendo wa mikopo kwa sekta binafsi, kiwango cha mitaji ya mabenki, uwiano kati ya mali inayoweza kubadilishwa kuwa fedha taslim na amana zinazoweza kuhitajika katika muda mfupi, na upatikanaji wa huduma za kifedha. Pale ambapo imedhihirika kuwa kuna upungufu wa ukwasi katika uchumi, Serikali kupitia Benki Kuu huchukua hatua mbalimbali za kisera kuchochea shughuli za kiuchumi. Hatua hizi ni pamoja na kuongeza ujazi wa fedha na kuboresha mazingira kwa sekta binafsi kukopa. Aidha, Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango inaweza kupunguza kodi na kuongeza matumizi ya Serikali.

    Hali ilivyo sasa

  5. Mheshimiwa Spika, hali ya baadhi ya vigezo vya ukwasi nchini ni kama ifuatavyo: kwa kutumia kigezo cha uwiano kati ya mali inayoweza kubadilishwa kuwa fedha taslim na amana zinazoweza kuhitajika kwa muda mfupi (Liquid assets to Demand Liabilities), uwiano huu ulikuwa asilimia 42.4 ukilinganishwa na asilimia 37.2 katika kipindi kama hicho mwaka 2015 na ikilinganishwa na uwiano wa chini unaohitajika kisheria wa asilimia 20. Amana za wateja katika mabenki zilipungua kidogo kutoka shilingi trilioni 20.73 mwezi Desemba 2015 kufikia shilingi trilioni 20.57 mwezi Septemba 2016. Miongoni mwa sababu zilizochangia kupungua kwa amana kwenye mabenki ni pamoja na uamuzi wa Serikali kuhamisha sehemu ya fedha za taasisi na mashirika ya umma kutoka mabenki ya biashara kwenda Benki Kuu ya Tanzania. Hata hivyo, amana za serikali kwenye mabenki ya biashara ni asilimia 3 tu ya amana zote za mabenki.  Aidha, jumla ya rasilimali za mabenki zimeendelea kuongezeka kutoka shilingi bilioni 26,917.2 mwezi Desemba 2015 hadi kufikia shilingi bilioni 27,978.2 mwezi Desemba 2016, sawa na ongezeko la asilimia 2.6.

    Mikopo kwa Sekta Binafsi

  6. Mheshimiwa Spika, mikopo kwa sekta binafsi iliongezeka kwa asilimia 7.2 katika kipindi cha mwaka ulioishia Desemba 2016 ikilinganishwa na ongezeko la asilimia 24.8 katika kipindi kama hicho mwaka 2015. Kupungua kwa kiwango cha ukuaji kulitokana na tahadhari iliyochukuliwa na mabenki kufuatia kuongezeka kwa mikopo chechefu kutoka asilimia 6.4 Desemba, 2015 hadi asilimia 9.5 Desemba, 2016.

  7. Mheshimiwa Spika, ni vema pia ieleweke kuwa kupungua kwa kasi ya kuongezeka kwa mikopo kwa sekta binafsi katika miezi ya hivi karibuni siyo kwa Tanzania pekee. Kwa mfano, kiwango cha ukuaji wa mikopo kwenda sekta binafsi katika nchi jirani ya Kenya kilipungua kutoka asilimia 19.7 kati ya Julai na Oktoba 2015 hadi kufikia asilimia 4.1 katika kipindi kama hicho mwaka 2016. Aidha, Nchini Uganda mikopo kwa sekta binafsi ilipungua kutoka asilimia 25.2 mwezi Septemba 2015 hadi asilimia -1 mwezi Septemba 2016. Pia mwenendo usioridhisha ulijitokeza katika mikopo chechefu katika nchi hizo jirani na kusababisha baadhi ya mabenki hususan Crane Bank ya Uganda kuwekwa chini ya uangalizi. Hali ni mbaya zaidi kwa nchi kama Nigeria na Ghana zinazouza mafuta.
  8. Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi wasiofikiwa na mabenki umeendelea kuongezeka kutokana na ubunifu wa mipango ya utoaji wa huduma za malipo ya rejareja kupitia simu za mikononi, pamoja na huduma za uwakala wa mabenki (agent banking services).

    Benki zilizopata msukosuko katika robo ya kwanza

  9. Mheshimiwa Spikakatika kipindi cha Julai – Desemba 2016, CRDB na TIB Development Bank zilipata hasara. Hasara ilisababishwa na tengo kwa ajili ya mikopo chechefu (provision for non performing loans). Aidha, Twiga Bancorp imewekwa chini ya uangalizi wa BOT, jambo ambalo si geni. Crane Bank Ltd ya Uganda iliwekwa chini ya usimamizi wa Benki Kuu ya nchi hiyo Oktoba 2016 kama ilivyokuwa Imperial Bank Kenya, Oktoba 2015. Licha ya hali hiyo, benki nyingi zikiwamo CRDB na TIB Development Bank, zimebaki kuwa na mitaji na ukwasi wa kutosha kwa mujibu wa Sheria. Aidha ni vema kukumbuka kwamba jumla ya benki na taasisi za fedha nchini kote ni 66 na zina matawi 783. Hivyo, kwa benki tatu (3) tu kupata msukosuko katika robo moja ya mwaka si sababu ya kuzua taharuki. Ikumbukwe pia kuwa hiki ni kipindi cha mpito na taasisi nyingi za Kibenki zilikuwa zinafanya tathmini ya utekelezaji wa maamuzi ya Serikali ya kuyataka Mashirika na Taasisi za umma kufungua akaunti za mapato BOT na kuhamishia amana za taasisi hizo hususan akiba za muda maalum (fixed deposit) kutoka kwenye mabenki ya biashara. Matarajio ya Serikali ni kuwa mara utaratibu mpya utakapozoeleka shughuli za kiuchumi zitaendelea katika uhalisia wake na Benki zitaendelea na huduma za mikopo na hivyo kuongeza ukwasi katika Uchumi.

    Uamuzi wa Serikali Kuzitaka Taasisi za Umma Kufungua Akaunti za Mapato Benki Kuu kama sababu ya Kupungua kwa Ukwasi katika uchumi.

  10. Mheshimiwa Spikani vyema Waheshimiwa Wabunge na jamii ya Watanzania ikafahamu kwamba akaunti ambazo fedha za mashirika zimehamishiwa Benki Kuu ni akaunti za kukusanya mapato tu na amana za muda maalum. Akaunti za matumizi bado ziko katika benki za biashara ili kuyawezesha mashirika kufanya malipo kupitia akaunti hizo. Hivyo, bado benki za biashara ni kiungo muhimu kati ya mashirika ya umma na watoa huduma kwa mashirika hayo. Hatua iliyochukuliwa na Serikali inalenga kuzisukuma benki za biashara kuchukua hatua za ziada kupanua huduma za kifedha hadi vijijini badala ya kujikita mijini zaidi kuhudumia makampuni makubwa (corporate sector) na kufanya biashara katika soko la dhamana na hati fungani za Serikali. Uamuzi huu umesaidia katika usimamizi wa mapato na matumizi ya Mashirika hayo na pia kurahisisha upatikanaji wa taarifa za fedha kupitia Benki Kuu. Aidha, Serikali imeacha kukopa fedha zake yenyewe na kwa gharama kubwa. Kwa kuwa amana za Serikali kwenye mabenki ya biashara ni sehemu ndogo tu (asilimia 3) ya amana zote za mabenki, madai kwamba uamuzi wa Serikali kuondoa fedha za mashirika na taasisi kwenda kwenye akaunti za mapato BOT umesababisha kupungua kwa ukwasi hayana uzito.

  11. Mheshimiwa Spika, naomba kusisistiza kuwa uamuzi wa Serikali kuzitaka taasisi za umma kufungua akaunti ya mapato Benki Kuu utaendelea kubaki kama ulivyo. Kwa kifupi, fedha hizi za umma zilikuwa zinatumika vibaya na mashirika lakini pia zilitumika kuikopesha Serikali fedha zake yenyewe kwa riba kubwa kupitia biashara ya dhamana na hati fungani za Serikali. Kasoro hiyo iliondoa motisha kwa mabenki ya biashara kupeleka huduma za kifedha vijijini na hata kukopesha sekta binafsi (crowding out credit to the private sector).

    Utoaji wa fedha kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kipindi cha Julai hadi Desemba, 2016

  12. Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kupeleka fedha katika Halmashauri zetu kwa kuwa ndiko utekelezaji wa miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi unapofanyika. Katika robo ya kwanza ya mwaka 2016/17, Serikali ilipeleka jumla ya shilingi bilioni 114.7 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na matumizi mengineyo. Aidha, katika robo ya pili ya mwaka, Serikali iliongeza mgao wa fedha zilizoenda kwenye Halmashauri ambapo kiasi cha shilingi bilioni 203.4 zilipelekwa. Serikali itaendelea kupeleka fedha katika halmashauri kwa kipindi kilichobaki kulingana na bajeti iliyoidhinishwa na Bunge lako Tukufu ili kuhakikisha ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za halmashauri za kuwahudumia wananchi.

    Ulipaji wa Madai Mbalimbali

  13. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Juni 30, 2016 kiasi cha shilingi bilioni 3, 113.7 ziliwasilishwa ikiwa ni madai ya wakandarasi, watumishi, wazabuni na watoa huduma. Baada ya Serikali kufanya uhakiki kupitia kwa Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali ilibainika kuwa madai halali yalikuwa shilingi bilioni 2,934.2 na madai yaliyokosa vielelezo na hivyo kukosa uhalali yalikuwa shilingi bilioni 179.5.

  14. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha nusu mwaka wa 2016/17, Serikali imelipa jumla ya shilingi bilioni 600.2. Kati ya kiasi hicho, shilingi bilioni 42.35 zilikuwa ni kwa ajili ya madai ya watumishi, shilingi bilioni 49.46 kwa ajili ya wazabuni, shilingi bilioni 11.2 kwa ajili ya watoa huduma, shilingi bilioni 30.0 kwa ajili ya madai ya vyombo vya ulinzi na usalama, na shilingi bilioni 467.2 kwa ajili ya wakandarasi mbalimbali ikijumuisha shilingi shilingi bilioni 2.0 kwa ajili ya makandarasi wa maghala na skimu za maji.

  15. Mheshimiwa Spika, kuhusu madeni ya pembejeo, Serikali bado inaendelea na uhakiki wa madeni hayo ili kubaini madai halali na yasiyo halali. Hata hivyo, katika kipindi cha Julai – Desemba, 2016 Serikali imetoa jumla ya shilingi bilioni 10.0 kwa ajili ya ruzuku ya pembejeo. Aidha, katika kuhakikisha madai ya wakandarasi, wazabuni, watumishi na watoa huduma wa ndani wanapewa kipaumbele, Serikali imeweka mkakati wa kutenga fedha kila mwezi ambapo mwezi Januari 2017 Serikali imetenga jumla shilingi bilioni 70.0.

    Jedwali Na. 2: Madeni yaliyolipwa kwa kipindi cha Julai - Desemba, 2016

    Jedwali Na. 3: Deni lililobaki baada ya malipo ya hadi Desemba 2016

    Mwenendo wa Deni la Taifa

  16. Mheshimiwa Spika, Deni la Taifa linajumuisha mikopo ambayo hukopwa na Serikali kutoka nje na ndani ya nchi kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo pamoja na kujaza nakisi ya bajeti. Deni la nje hukopwa kutoka kwenye taasisi za kifedha kama vile Benki ya Dunia, nchi Wahisani na pia kutoka kwenye benki za biashara wakati deni la ndani linapatikana kwa kuuzwa kwa dhamana za Serikali (treasury bills) na hatifungani (Treasury bonds), mikopo kutoka Benki Kuu ya Tanzania na benki za biashara za ndani.

  17. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia Deni la Taifa kwa kuzingatia Sheria ya Mikopo, Dhamana, na Misaada SURA 134.  Aidha, katika kuhakikisha kuwa Deni la Taifa linasimamiwa kikamilifu Serikali inakamilisha mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Mikopo, Dhamana na Misaada SURA 134 ili kuimarisha usimamizi wa Deni la Taifa.

  18. Mheshimiwa Spikahadi kufikia Desemba, 2016, Deni la Taifa likijumuisha deni la ndani na la nje lilifikia Dola za Kimarekani milioni 19,021.9 (debt stock) ikilinganishwa na Dola za Kimarekani milioni 18,459.3 Juni, 2016 ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 3.05. Kiasi hiki cha deni hakijumuishi deni la Mifuko ya Hifadhi ya Jamii linalokadiriwa kufikia Dola za Kimarekani milioni 1,725.8 ingawaje deni hilo limezingatiwa katika tathmini ya uhimilivu wa deni la Taifa.

  19. Mheshimiwa Spika, ongezeko la deni hilo limetokana  na mikopo iliyopo na mipya iliyopokelewa na Serikali na ambayo bado haijaiva kutoka mikopo ya ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo kama vile reli ya Tazara, daraja la Kikwete mto - Malagarasi, barabara ya Morogoro – Dodoma, barabara ya Dodoma – Singida – Arusha, barabara ya Mwanza – Bukoba, mradi wa Maji ziwa Victoria, Bomba la Gesi Mtwara – Dar es Salaam, barabara ya Dodoma - Singida – Mwanza, miradi ya umeme Kinyerezi I & II, Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano n.k. Miradi ambayo iligharamiwa na mikopo hiyo imeelezewa kwa kina katika kitabu cha Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2017/18 na katika kitabu cha Uchambuzi wa Deni la Taifa pamoja na miradi inayofadhiliwa na deni hilo. Pamoja na miradi iliyotajwa, naomba kuweka mezani taarifa ya Agosti,2016 ya uchambuzi wa Deni la Taifa na miradi yote iliyofadhiliwa na deni hilo tangu uhuru.

    Ulipaji wa Deni la Taifa

  20. Mheshimiwa Spika, ulipaji wa Deni la Taifa hauangalii ukubwa wa deni lililopo (stock of debt) bali kadri deni linavyoiva (debt maturity). Hali ilivyo sasa sehemu kubwa ya Deni la Taifa linaiva kwa kipindi cha muda mrefu (long term maturity). Kutokana na hali hiyo, kwa wastani (average time to maturity) wa deni lililopo sasa litaiva katika kipindi cha miaka isiyopungua 11.9. Hali hii inaashiria kwamba athari zake kwenye bajeti ziko chini (low refinance risk).

  21. Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikilipa madeni ya nje na ndani kwa mujibu wa mikataba. Katika kipindi cha kuanzia Julai, 2016 hadi kufikia Desemba, 2016 Serikali ilitumia jumla ya shilingi bilioni 2,570.1 kulipia madeni ya ndani na nje yaliyoiva. Kati ya kiasi hicho, malipo ya deni la ndani ni shilingi bilioni 1,822.3 na deni la nje ni shilingi bilioni 747.8. Malipo ya deni la ndani yanajumuisha malipo ya mtaji (rollover) ya shilingi bilioni 1,367.1 na malipo ya riba ya shilingi bilioni 455.2

  22. Mheshimiwa Spika, dhamira ya Serikali ni kuendelea kulipa kwa wakati mikopo yote ya nje inayoiva kwa mujibu wa mikataba. Aidha, Serikali itaendelea na utaratibu wa kukopa kwa ajili ya kulipa mtaji kwa amana zinazoiva (rollover of principal maturities of T-bonds and T-bills). Lengo la kuendelea na utaratibu huo (rollover) ni kutoa ahueni kwenye bajeti ya kila mwaka husika na ni utaratibu wa kawaida unaotumika na nchi nyingi duniani.



  1. Mheshimiwa Spika, athari za kutolipa deni kwa mujibu wa mikataba ni zifuatazo: nchi itahatarisha mahusiano yaliyopo kati yake na nchi wahisani, taasisi za fedha za kimataifa na mabenki ya nje; nchi inaweza kushtakiwa kwenye mahakama za kimataifa na kuisababishia hasara na kutopata mikopo; kukamatwa kwa mali zake (Assets) zilizopo nje na ndani ili kulipia madeni ambayo yatakuwa hayajalipwa; na kulipa gharama za ziada kama adhabu (penalty) kulingana na makubaliano na hivyo kuongeza mzigo wa Deni kwa Taifa.



  1. Mheshimiwa Spika, naomba ifahamike kuwa malipo yote ya mikopo ya ndani na nje hukasimiwa katika Fungu namba 22. Kwa kuzingatia utaratibu wa kibajeti, matumizi yote yaliyokasimiwa katika Fungu hili ni matumizi yasiyo epukika (first charge). Kutokana na utaratibu huo wa kibajeti na athari nilizozieleza hapo awali za kutokulipa mikopo kulingana na mikataba, malipo yote ya mikopo ya ndani na nje hulipwa kwa wakati pindi yanapoiva. Aidha, kwa upande wa madai ya ndani ya makandarasi, wazabuni, watumishi na watoa huduma, malipo yake hukasimiwa kwenye mafungu mengine ya Wizara, Mikoa na Halmashauri ambayo hayapo katika kundi la matumizi yasiyo epukika. Hivyo, madai haya hulipwa baada ya uhakiki kukamilika.

  2. Mheshimiwa Spika, sambamba na ulipaji wa Deni la Taifa, Serikali imeendelea kugharamia utoaji wa huduma nyingine za jamii na utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kwa mfano, katika kipindi cha Julai hadi Desemba, 2016 Serikali iligharamia yafuatayo: Ununuzi wa ndege mbili za Serikali na malipo ya awali ya ununuzi wa ndege 4 shilingi bilioni 234.937; Upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Dodoma na Mwanza Shilingi bilioni 12.353; Usambazaji wa umeme vijijini Shilingi bilioni 267.529; Ujenzi na ukarabati wa barabara Shilingi bilioni 916.779; na Usambazaji wa maji vijijini na mijini Shilingi bilioni 165.213. Aidha, Serikali imeendelea kugharamia mikopo kwa wanafunzi wa Elimu ya Juu Shilingi bilioni 277.534; Mfuko wa Reli Shilingi bilioni 58.04942; Uboreshaji wa huduma za afya katika ngazi zote ikiwemo ununuzi wa dawa na vifaa tiba Shilingi bilioni 235.229; Mitihani Shilingi bilioni 64.796; Kugharamia vyombo vya ulinzi na usalama shilingi bilioni 388.4; na Chakula cha wafungwa Shilingi bilioni 9.0.



  1. Mheshimiwa Spika, mahitaji mengine yaliyopewa kipaumbele ni elimu msingi bila malipo Shilingi bilioni 124.851 (kwa kutenga shilingi bilioni 18.777 kila mwezi);  Ruzuku ya pembejeo shilingi bilioni 10.00; Ununuzi wa chakula cha Hifadhi ya Taifa shilingi biliioni 9.00; Deni la kuchapisha Vitabu vya Hati za Kusafiria Shilingi 2.569; Uendeshaji wa vikao vya Kamati za Kudumu za Bunge, Mkutano wa Bunge, Posho ya Jimbo kwa Wabunge pamoja na shughuli za Mfuko wa Bunge Shilingi bilioni 35,262; Michango ya Taasisi na Jumuiya za Kimataifa Shilingi billion 9.8; Ruzuku ya Vyama vya Siasa Shilingi bilioni 8.601; Ujenzi wa majengo ya utawala kwenye halmashauri mpya bilioni 10; Kugharamia balozi zetu nje ya nchi shilingi bilioni 40.7; Ujenzi na ukarabati wa ofisi za Halmashauri Shilingi bilioni 30.10; Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo Tanzania bara Shilingi bilioni 9.0 na Tanzania Zanzibar ni shilingi bilioni 1.4; na Uboreshaji wa miundombinu ya shule za wanafunzi wenye mahitaji maalum Shilingi bilioni 2.5.

    Tathmini ya Uhimilivu wa Deni la Taifa
  2. Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mikopo Dhamana na Misaada Sura 134, Serikali inawajibu wa kufanya tathimini ya uhimilivu wa deni (Debt Sustainability Analysis) kila mwaka ili kupima hali ya deni  na uhimilivu wake kwa kipindi cha muda mfupi, wa kati na mrefu. Kwa kuzingatia matakwa ya Sheria hiyo timu ya wataalamu wamekamilisha tathmini ya uhimilivu wa deni la Taifa kwa mwaka 2016/17. Matokeo ya tathmini hiyo yanaonesha kuwa deni ni himilivu kwa muda mfupi, wa kati na mrefu. Matokeo hayo yanafanana na yale yaliyotolewa katika taarifa ya IMF ya uhimilivu wa deni la Taifa iliyotolewa Juni 2016– United Republic of Tanzania Staff report for the 2016 Article IV  Consultation, and Fourth Review under Policy Support Instrument ambayo ipo kwenye tovuti ya IMF.

  3. Mheshimiwa Spika, katika tathmini iliyofanyika Novemba 2016, viashiria vinaonesha kuwa: thamani ya sasa ya jumla ya deni la Taifa (Present Value of Total Public Debt) kwa Pato la Taifa ni asilimia 34.2 ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 56, thamani ya sasa ya Deni la nje pekee (Present Value of External Debt)  kwa Pato la Taifa ni asilimia 19.9 ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 40; thamani ya sasa ya  deni la nje kwa mauzo ya nje ni asilimia 97.7 ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 150; na thamani ya sasa ya deni la nje kwa mapato ya ndani ni asilimia 145.3 ikilinganishwa na ukomo wa asilimi 250.

  4. Mheshimiwa Spika: kazi ya viashiria hivyo vinne ni kupima uwezo wa nchi kukopa (solvency threshhold). Viashiria vilivyobaki vinapima uwezo wa nchi kulipa deni (Liquidity Indicators). Kutokana na tathimini,  ulipaji wa deni la nje kwa kutumia mapato ya ndani umefikia asilimia 11.5 ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 20 na Ulipaji wa deni la nje kwa kutumia mauzo ya bidhaa nje ni asilimia 7.8 ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 20. Kwa kuzingatia vigezo hivyo, Tanzania bado ina uwezo wa kuendelea kukopa toka ndani na nje ya nchi ili kugharamia shughuli zake za maendeleo na pia ina uwezo wa kulipa mikopo inayoiva kwa kutumia mapato yake ya ndani na nje kwa wakati.

    Jedwali Na. 4: Viashiria vya Uhimilivu wa Deni Taifa


VIASHIRIA VYA DENI LA NJE

2015/16

2016/17

2017/18

2020/21

2025/26

2035/36

Ukomo

Deni la nje (PV ) /Pato la Taifa

19.9

19

18.8

20.1

18.9

14.2

40

Deni la nje  (PV) / uuzaji wa bidhaa nje

97.7

94.2

98.2

107.4

95.5

71.0

150

Deni deni la nje (PV) / Mapato ya ndani

145.3

111.46

114.3

98.7

91.8

68.39

250

Ulipaji wa deni la nje/Uuzaji wa bidhaa nje

7.8

9.2

8.4

8.0

7.9

8.0

20

Ulipaji wa deni/ Mapato ya ndani

11.5

11.0

9.7

7.3

7.6

7.7

20

VIASHIRIA VYA DENI LA NJE NA LA NDANI (Total Debt)





Deni (PV) /Pato la Taifa

34.2

32.5

31.2

32.7

29.4

23.3

56

Deni (PV) / Mapato ya ndani

30.8

21.1

23.4

16.9

16.6

16.1





  1. Mheshimiwa Spika, kutokana na muundo wa deni la Tanzania (debt structure) sehemu kubwa ya madeni yake yanaiva kwa muda mrefu (miaka 5 hadi 50). Hivyo, upimaji wa deni la Taifa huangaliwa kwa kutumia thamani ya sasa ya deni (Present value of debt) badala ya kutumia thamani halisi ya deni (nominal value of debt) hii inaiwezesha tathmini iweze kufanyika kwa madeni yanayoiva kwa muda mrefu kinyume na thamani halisi ya deni kwa pato la Taifa (nominal value of debt to GDP), ambayo inaangalia hali ya deni kwa muda mfupiKwa kuzingatia hali hiyo, viashiria vilivyooneshwa hapo juu ndio viashiria sahihi vilivyokubalika kimataifa katika upimaji wa uhimilivu wa Deni la Taifa.

  2. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia vigezo hivyo, uwiano wa deni lote la ndani na nje kwa thamani ya sasa kwa pato la Taifa (PV of total public debt/GDP) kwa mwaka 2015/16 Kenya ilikuwa asilimia 45.6, Tanzania asilimia 34.2, Uganda asilimia 24.1, na Rwanda asilimia 22.7.  Vile vile, uwiano wa deni la nje kwa thamani ya sasa kwa Pato la Taifa: Kenya ilikuwa asilimia 19.4; Tanzania asilimia 19.9; Uganda asilimia 10.7; Rwanda  asilimia 17.3 (PV of external debt/GDP) ambavyo vyote bado viko chini ya ukomo.
  3. Mheshimiwa Spika, vigezo vinavyoelezwa na baadhi ya wadau kama Mhe. Kishoa kuhusu uhimilivu wa deni la Taifa kwa kutumia uwiano wa nominal debt to GDP siyo sahihi kwa kuwa upimaji wa uhimilivu wa deni la Tanzania sehemu kubwa ya deni lake linaiva katika kipindi cha muda mrefu. Vigezo vinavyotumia uwiano wa  nominal debt to GDP  ni vizuri kwa kuangalia mwenendo wa deni badala ya uhimilivu wa deni.

  4. Mheshimiwa Spika, taarifa ya IMF review mission iliyotolewa Oktoba 31, 2016 inasema hivi naomba kunukuu:

    ‘‘The mission held discussions on how to address these macroeconomic challlenges. In particular, the importance of mobilising external financing to step up the pace of planned capital spending. Tanzania is at low risk of external debt distress and has room to borrow externally on concessional and nonconcessional terms to meet its financing needs….It also recommended …acquiring a sovereign credit rating to expand Tanzania’s opportunities to borrow abroad…’’

  5. Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kwamba Deni la Taifa linadhibitiwa na linaendelea kuwa himilivu, Serikali inatoa kipaumbele kwa mikopo yenye masharti nafuu. Hata hivyo, pamoja na mikopo hiyo kuwa na masharti nafuu ya kifedha, lakini kuna masharti mengine ambayo yanagusa maslahi ya nchi na hivyo kusababisha kuchelewa au kushindwa kuchukua mikopo hiyo. Kwa mfano, masharti ya mkopo kwa ajili undelezaji wa Bandari ya Dar es salaam kutoka Benki ya Dunia ambapo serikali inasita kuyaridhia kutokana na maslahi ya taifa.

  6. Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kwamba Deni la Taifa linadhibitiwa na linaendelea kuwa himilivu, Serikali inatekeleza mikakati ifuatayo:

  1. Kuhakikisha kwamba mikopo inayopewa kipaumbele ni ile yenye masharti nafuu, na kwamba mikopo yote yenye masharti ya kibiashara inakopwa kwa uangalifu mkubwa ikiwemo kuhakikisha kwamba mikopo hiyo inatumika kwenye maeneo ambayo yana vichocheo vya ukuaji wa uchumi;
  2. Kuboresha mikakati ya kukusanya kodi ili kuhakikisha sehemu kubwa ya bajeti yetu inagharamiwa na mapato ya ndani pamoja na kupunguza matumizi yanayoweza kuepukika;
  3. Kusimamisha kabisa utoaji wa Dhamana za Serikali kwa Taasisi za Serikali ambazo zinategemea ruzuku kujiendesha. Hii itasaidia kupunguza deni linalotokana na taasisi hizo kushindwa kulipa madeni hayo; na
  4. Kuimarisha Usimamizi wa deni kwa kuwa na Idara maalum ndani ya Wizara ya Fedha na Mipango itakayokuwa na jukumu la kusimamia deni la Taifa. Aidha, Serikali inarekebisha Sheria ya Mikopo, Dhamana na Misaada ili iweze kuwiana na hali ya sasa.


  1. Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa Deni la Taifa, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali anaendelea kufanya ukaguzi maalum na yupo katika hatua za mwisho za kukamilisha taarifa ambayo itatoa hali halisi ya Deni la Taifa.


Hatua iliyofikiwa kwa makampuni ya simu kujisajili katika soko la hisa

  1. Mheshimiwa Spika; kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2016 kifungu cha 26 kinaeleza kuwa:

  1. Makumpuni ya mawasiliano yenye leseni ya kujenga miundombinu ya mawasiliano (Network Facilities) na yenye leseni ya kutoa huduma za mawasiliano (Network Services or Application Services) yawe na umiliki wa watanzania usiopungua asilimia 25 ya mtaji wa kampuni katika kipindi chote cha uhai wa leseni yake;

  2. Makampuni yenye leseni ya huduma ya utangazaji (Content Service Licensee) yawe na umiliki wa kitanzania usiopungua asilimia 51 ya mtaji katika kipindi chote cha leseni;

  3. Kiwango cha chini cha asilimia 25 ya umiliki upatikane kupitia umiliki wa umma kwa mujibu ya Sheria ya Soko la mitaji na Dhamana;

  4. Makampuni yaliyotajwa hapo juu ambayo tayari yalikuwa yanafanya kazi nchini kabla ya tarehe 01 Julai, 2016, yanatakiwa yajisajili katika soko la hisa ndani ya kipindi cha miezi 6 kuanzia tarehe 1 Julai, 2016; na

  5. Makampuni ambayo yatasajiliwa nchini kuanzia tarehe 01 Julai, 2016 yatatakiwa kujisajili katika soko la hisa ndani ya miaka miwili toka kuanzishwa kwake.



  1. Mheshimiwa Spika; kuna jumla ya kampuni 80 zilizopewa leseni za miundombinu ya mawasiliano na huduma za mawasiliano ambazo zinahusika na Sheria hii. Hadi tarehe 03 Januari, 2017 kwa mujibu wa taarifa ya Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) ni Kampuni tatu tu za VODACOM, AIRTEL na TIGO ndizo zilizowasilisha nyaraka za usajili ambapo kampuni ya VODACOM ndiyo iliyowasilisha nyaraka zilizokamilika na kampuni nyingine ziliwasilisha nyaraka zenye mapungufu. Kampuni nyingine zilitoa taarifa kuwa wapo katika hatua mbalimbali za kuorodhesha hisa zao ikiwa ni pamoja na kupata ushauri kutoka CMSA na kwa wataalamu wa masuala ya kuandaa hati maalum za kuorodheshwa kwenye soko la hisa.

  2. Mheshimiwa Spika;  mnamo tarehe 13 Januari, 2017, Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) kama msimamizi wa Sheria ya Mawasiliano ya Kieletroniki na Posta (EPOCA) ilitoa notisi kwa kampuni za simu kwa mujibu wa kifungu cha 22 cha EPOCA, na kuziagiza kampuni za simu kuorodhesha hisa zao kwenye soko la hisa, katika kipindi cha siku 30. Baada ya siku 30 kupita toka notisi kutolewa, TCRA itachukua hatua za kisheria dhidi ya kampuni ambazo hazijakamilisha usajili wa hisa zao.



Wafanyabiashara kusita kuagiza bidhaa kutoka nje ya Nchi kwa kigezo cha kwamba uchumi wa Nchi haueleweki.



  1. Mheshimiwa Spikakatika kipindi cha Julai hadi Desemba 2016, thamani ya uagizaji wa bidhaa ilipungua kwa asilimia 3.9 kufikia Dola za Kimarekani milioni 4,422.4 ikilinganishwa na Dola za Kimarekani milioni 4,603.7. Hata hivyo, kupungua kwa uagizaji wa bidhaa hakuwezi kuhusishwa moja kwa moja na wasiwasi walio nao wafanyabiashara kwamba uchumi wa nchi haueleweki. Zipo sababu kadhaa za kupungua kwa uagizaji ikiwemo hatua za kiutawala zilizochukuliwa na Serikali kudhibiti mianya ya biashara ya magendo.

  2. Mheshimiwa Spikakuzibwa kwa mianya hiyo kumesababisha upungufu wa bidhaa ambazo zilikuwa zinauzwa kwa bei ya chini kutokana na kutokutozwa kodi stahiki. Wafanyabiashara ambao wanasemekana kusita kuagiza bidhaa kutoka nje ya nchi kwa kigezo cha kwamba uchumi wa nchi haueleweki, baadhi yao ni wale waliokuwa wanatumia mwanya wa kukwepa kulipa kodi ambao sasa umezibwa kwa kiasi kikubwa. Hivyo, sababu za baadhi ya wafanyabiashara kusita kuagiza mizigo zinaweza kuwa ni pamoja na kushindwa kuingiza bidhaa nchini bila kulipa kodi stahiki, kushindwa kulipa au kulipwa madeni, kubadilisha aina ya biashara, kushindwa kusimamia biashara, gharama kubwa za uendeshaji, kuibuka kwa washindani wa kibiashara wenye nguvu au huduma bora zaidi n.k. Ni matarajio ya Serikali kwamba  wafanyabiashara na watanzania kwa ujumla watazoea mfumo huu wa kulipa kodi stahiki na hivyo kuongeza uagizaji wa bidhaa na huduma. Serikali itaendelea kuboresha mfumo wa kodi ili uwe rafiki zaidi kwa wafanyabiashara.

    Hitimisho

  3. Mheshimiwa Spikakama tulivyoona katika viashiria mbalimbali vya kiuchumi, uchumi wa Tanzania uko imara na tulivu, mfumuko wa bei umedhibitiwa katika wigo wa tarakimu moja, Benki zetu bado zina ukwasi wa kutosha kuweza kukopesha wananchi na Deni la Taifa linaendelea kuwa himilivu. Taarifa huru ya IMF iliyotolewa tarehe 9 Januari, 2017 inathibitisha ukweli huu kwa kusema:

    ‘‘Tanzania’s macroeconomic performance remains strong. Economic growth was robust during the first half of 2016 and is projected to remain at about 7 percent this fiscal year. Inflation came down below the authorities’ target of 5 percent and is expected to remain close to the target, while the external current account deficit was revised down on account of lower imports of capital goods.”

  4. Mheshimiwa Spikaziko changamoto kadhaa ambazo Serikali inaendelea kuzifanyia kazi hususan zile ambazo zipo ndani ya uwezo wa Serikali. Ninawasihi Waheshimiwa Wabunge tushirikiane kwa pamoja katika masuala yote ya maendeleo ya nchi yetu na tutumie taarifa rasmi katika kuwafikishia wananchi ujumbe ulio sahihi. Aidha, kama nilivyoeleza awali, napenda kuwahakikishia waheshimiwa wabunge na watanzania kwa ujumla kwamba uchumi wetu ni tulivu, uko imara na tunategemea utaendelea kuwa hivyo katika kipindi cha muda wa kati. Nirudie kwa kuwahakikishia kuwa hakuna mdororo wa uchumi nchini.

  5. Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.